Sponsored Community Message Browse Free. Go deeper with Full Access. Free visitors can browse public knowledge. Full Access unlocks participation, member areas, and an ad-free experience.

Swahili Poems-gctid30369

Started by KaNisa, Aug 13, 2008, 05:28 AM

Previous topic - Next topic
Swahili Poems

Kitandawili Natowa
 
 Date: July 1, 2000
 Author: Hashil S. Hashil, Denmark.
 
    1. Natowa kitandawili / mwenye jawabu kutowa
       Wako watu sura mbili / majaraha yasopowa
       Kuchupa kwao kuwili / nyoyo zao zaunguwa
       Watakayo ni muhali / milele hayatokuwa.
    2. Akili zao ni ghali / kutu zinawasumbuwa
       Wapigana na makali / mwenye fani hupekuwa
       Warejea ya awali / hawavuki zao puwa
       Wala hawana muhali / wamegeuka viluwa.
    3. Wanapeta pili pili / ungó wao chandaruwa
       Upungufu wa akili / ukweli kuutambuwa
       Wasemavyo waawali / wengine wajisumbuwa
       Hatari yawakabili / kuviwasha vilopowa.
    4. Mkahawa sihoteli / kushindana kutambuwa
       Dibeti zisoukweli / mtuno wakitumbuwa
       Kisu kutiwa makali / mwerevu anang´amuwa
       Ukweli muukubali / mwiko mwenziwe upawa.
 
 Kitandawili (Jibu)
 
 Date: July 1, 2000
 Author: Hassan O. Ali, Ottawa, Canada.
 
    1. Watu wenye sura mbili, unao wasimulia
       Si watu ni makubeli, wako tayari kuua
       Tukae nao kwa mbali, roho wasije zitoa
       Watu wasio murua, ni maadui wa kweli.
    2. Wasifu wao tumbili, kila mti wachupia
       Vipando vyetu halali, haweshi kuvivamia
       Tena wafanya kejeli, majumbani waingia
       Watu wasio murua, ni maadui wa kweli.
    3. Hawajali hawabali, wendekeza ya dunia
       Nyoyo zao za jabali, imani 'mewapotea
       Wanajikumbizia mali, nundu zao za ngamia
       Watu wasio murua, ni maadui wa kweli.
    4. Asiyemcha Jalali, Muumba wetu Jalia
       Hafai hastahili, kuwaongoza raia
       Isiwe mara ya pili, fursa kumuachia
       Watu wasio murua, ni maadui wa kweli.
    5. Beti tano ni kamili, kuongeza sina nia
       Kwa chako kitendawili, jibu nimekutolea
       Nambie ewe Hashili, kama nimekipatia
       Watu wasio murua, ni maadui wa kweli.
 
 Pakacha Pakachuka
 
 Date: May 24, 2002
 Author: Hassan O. Ali, Ottawa, Canada.
 
    1. Pakacha waniweka, roho juu
       Pakacha kila mwaka, hata huu!
       Pakacha wanitaka, niwe zuu?
       Pakacha pakachuka, chini puu!
    2. Pakacha nadhikika, dhiki kuu!
       Pakacha ninanuka, na kupuu
       Pakacha wanicheka, sana tuu!
       Pakacha pakachuka, chini puu!
    3. Pakacha umeruka, kichuguu
       Pakacha hujavuka, lima kuu
       Pakacha 'tachauka, chau chau
       Pakacha pakachuka, chini puu!
    4. Pakacha sina shaka, si kifuu
       Pakacha asotaka, la mkuu
       Pakacha huvunjika, lake guu
       Pakacha pakachuka, chini puu!
 
 Pakacha Pakachuka ... (jibu)
 
 Date: May 24, 2002
 Author: Bakari A. Ali, Reading, U.K.
 
    1. Tungo ni safi nzuri, ahsantuu
       Utunzi huna dosari, wewe juu
       Waenda njema safari, ya majuu
       Hassani wewe hodari, ni mkuu
    2. Beti zanukia wazi, karafuu
       Twafurahia ujuzi, ulio juu
       Furaha kubwa azizi, sikukuu
       Mkono wenye pongezi, shika huu
 
 Pakacha Pakachuka ... (jibu)
 
 Date: May 24, 2002
 Author: Hashil S. Hashil, Denmark.
 
    1. Pakacha parachuka, wajikuta chini juu
       Pakacha lakucheka, mzegazeka nafuu
       Pakacha kunited snakesrifika, zambarau sio fuu
       Pakacha towa talaka, ndio siri ya kifuu
    2. Pakacha ni kichaka, cha mbuni vitu kuviacha wazi
       Pakacha mashaka, wengi wauza mbaazi
       Pakacha kushilanga muafaka, shabaha kupanda ngazi
       Pakacha kuliamini ni shaka, lageuka utelezi
    3. Pakacha nakunasihi, fujo zako kuziacha
       Pakacha huzimi wala huwashi, wajijua umechacha
       Pakacha kipimo chako ni pishi,wengine watoto pacha
       Pakacha ubani wako mafushi, mara nyengine mchicha
    4. Pakacha kujihashuwa uwache, mara hii utadunda
       Pakacha makarara kwako cheche, mnyama wako ni punda
       pakacha gari lako ni mkweche, wapakia vilovunda
       Pakacha miye si cheche, ni sungura kwenye sanda.
 
 Pakacha Pakachuka ... (jibu)
 
 Date: May 25, 2002
 Author: Ally bin Aboubakar, ukkk, U.K.
 
    1. Wallahi nafurahika, ushairi kuushika,
       Malumbano kuyateka, na nyoyo kuburudika,
       Ila Pakacha nateta, jawabu hatujalipata,
       Pakacha hili nlipi, la Canada au Pemba?
    2. Dr.nakukumbusha,pakacha la kwenu Pemba,
       Muhogo na wake pweza,jioni utajitweka,
       Masheli ya kupwaza,si haba utajitwika,
       Pakacha hili nlipi,mbona hwelitaja?
    3. Karafuu hichumia, na mpeta kuokotea,
       Leo mbona mwalinunia, pakacha hili la kujivunia,
       Wallahi najivunia, mipesa nejichumia,
       Dr.Hassan hebu nambia, kabla sijakufokea,
    4. Komputa hutaitia, ndani ya pakacha nakwambia,
       Ila ndio tweanzia, karafuu na kijio kutafutia,
       Hebu leo twambie, huko canada lipo hilo Pakacha
       Au nlile la aslia , Pemba na Unguja lanukia?
 
 N'na Paka Guniani
 
 Date: October 25, 2000
 Author: Hassan O. Ali
 
    1. Sitathubutu kusema, nimeshakula yamini
       Mchota maji kisima, hata iwe muadhini
       Hatanitoa kalima, wala hatanizaini
       N'na paka guniani, sitathubutu kusema
    2. Paka huyu kisirani, si paka ni ngawa-nyumba
       Avuua kaangoni, mara akinunited snakes vumba
       Jeleko la kizamani, alitipa kama pamba
       N'na paka guniani, sitathubutu kusema
    3. Si paka ni subiani, jini amepigwa chapa
       Usipokaa makini, mara hukwendesha kapa
       Ndio hasema sineni, kanishinda namtupa
       N'na paka guniani, sitathubutu kusema
    4. Sitasema akarudi, akazidi kunitimba
       Nimeifanya juhudi, mwituni nenda msumba
       Hutendwa lisilo budi, mdomo ninaufumba
       N'na paka guniani, sitathubutu kusema
 
 Heko Kwa Bwana Hassani ... (jibu)
 
 Date: October 25, 2000
 Author: Ahmed Rashid
 
    1. Japo paka subiani, shetani wa ujinini,
       Sasa yuko hatarini, simtoe guniani,
       Enenda naye porini, umfukie shimoni,
       Heko kwa Bwana Hassani, kalitupe paka shume.
    2. Kalitupe paka shume, likatoweke mwituni,
       Litupe lisisimame, limetuchosha nyoyoni,
       Uhakika tuuseme, ni paka shume ja nyani,
       Heko kwa Bwana Hassani, kalitupe paka shume.
    3. Paka hili jizi sana, masinzi tele usoni,
       Mbinuze ni nyingi sana, kuiba nyama jikoni.
       Hata Hassani kinena, shume harudi nyumbani,
       Sema siogope shume, shume harudi nyumbani.
    4. Kusema usiogope, yanene yote wavuni,
       Na changa moto tukupe, uyatoe ya moyoni,
       Kwa pamoja tulitupe, shume lilo guniani,
       Heko kwa Bwana Hassani, kalitupe paka shume.
"Isn't it sad how some people's grip on their lives is so precarious that they'll embrace any preposterous delusion rather than face an occasional bleak truth?"